Serikali wilayani Bunda yaachia NGO'S kuwahudumia wenye ukimwi. - Mazingira FM

Mazingira Fm Live

Breaking News

Tuesday 20 February 2018

Serikali wilayani Bunda yaachia NGO'S kuwahudumia wenye ukimwi.



MRATIBU  wa shughuli  za UKIMWI  katika halmashauri ya wilaya ya Bunda mkoani  Mara, Vitus  Gwanko amedai serikali  kwa sasa  haina bajeti  ya  kuwahudumia wananchi  wa kawaida wanaoishi  na virusi  vya UKIMWI badala yake  shughuli hiyo imeachiwa  mashirika yasiyo ya kiserikali(NGO’s).

Akijibu  hoja za madiwani waliotaka kujua sababu za halmashauri  hiyo kutokuwa  na  bajeti  ya kuwahudumia   watu wa kawaida  wanaoishi na VVU, Gwanko alidai  kwa mwongozo waliyo nayo  sasa halmashauri  imeweka bajeti  ya  kuwahudumia  watumishi  wa umma pekee  wanaoishi  na VVU  ndani  ya  halmashauri husika na sio watu wa kawaida.

Kwa mujibu  wa Gwanko, halmashauri ya wilaya ya Bunda kwa sasa haina bajeti  ya kuwahudumia waviu, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi  juu ya UKIMWI, upatikanaji  wa madawa  ya ARV’s na huduma zingine.

Alidai  awali halmashauri  zilikuwa na bajeti hiyo  kutoka tume ya kudhibiti Ukimwi nchini(TACAIDS) ambayo ilikuwa ikipata fedha toka kwa wafadhili na kwamba tangu wafadhili  wasitishe mradi huo, huduma ya kutoa  madawa ya kufumbaza virusi(ARV’s) na huduma zingine  kwa WAVIU imebaki kwa mashirika na asasi  za kiraia na sio serikali.

Naye ofisa utumishi  katika halmashauri hiyo, Bakarani Oriwo alieleza kuwa bajeti  iliyopo katika halmashauri  yake inahusu WAVIU ambao ni watumishi  wa umma na kwamba hiyo inatokana na agizo la serikali  la kuhakikisha kuwa  wafanyakazi  wanaoishi  na VVU wanapewa huduma stahiki katika vituo vyao vya kazi na sio wananchi wa kawaida.

“Mwananchi  wa kawaida anapata huduma  hizi  bure kutoka  mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo  yanafanyakazi hii kwa mujibu  wa sheria nchini kote, lakini sisi katika bajeti yetu haijatuelekeza kuwahudumia WAVIU  ambao sio watumishi  wa umma” alisisitiza Oriwo.

Hata hivyo  baadhi  ya madiwani  waliitaka serikali  kuweka mpango  wa kutenga bajeti  kwa ajili ya wananchi  wanaoishi na VVU huku wakitoa tahadhari kuwa siku mashirika  na asasi za kiraia zitakapositisha  shughuli zao za kuwahudumia WAVIU  kutatokea shida kubwa nchini.

Madiwani hao walisema hivi sasa  WAVIU wengi wanakosa  huduma  ya ushauri nasaha, pamoja na kutumia muda mwingi katika kufuatialia huduma hizo ikiwa ni pamoja na ARV’s).


Walisema si vyema serikali kuonesha upendeleo wa kutenga bajeti  kwa ajili ya kuwahudumia  WAVIU ambao ni watumishi  wa umma pekee  huku wananchi  wenyewe wakitegemea hisani  toka kwa wafadhili.

Mjadala huo ulikuja baada ya Mwenyekiti  wa kamati ya UKIMWI katika halmashauri hiyo, Simba Mramba  kulilieleza baraza la madiwani kuwa halmashauri hiyo imetenga jumla ya shilingi milioni 4 tu kwa ajili ya kuwahudumia  wafanyakazi  wanaoishi  na VVU katika mwaka wa fedha 2018/2019.

No comments:

Post a Comment