Mkuu wa wilaya ya Bunda asema bila kupitia mafunzo ya mgambo hupati nafasi ya JKT -Bunda Mara - Mazingira FM

Mazingira Fm Live

Breaking News

Tuesday 13 March 2018

Mkuu wa wilaya ya Bunda asema bila kupitia mafunzo ya mgambo hupati nafasi ya JKT -Bunda Mara



SERIKALI wilayani Bunda mkoani Mara, imesema kuanzia mwaka huu wanaotakiwa kujiunga na mafunzo ya jeshi la akiba(Mgambo) ni sharti wawe na sare ya jeshi hilo linalogharimu kiasi cha shilingi 139,000 vinginevyo hawatachaguliwa kupata mafunzo hayo.

Sare hizo ni suruali, Jaketi na kofia(sh.50,000), T-shirt(sh.7,500), Viatu(sh.65,000) na mkanda(sh.15,000) na kwamba fedha hizo zilipwe katika akaunti ya benki ya CRDB Suma JKT, lenye jina “National Service Garment Factory” N0.0150238972300. 

Akielezea utaratibu wa kuomba mafunzo hayo mwaka huu kwa waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa wilaya ya Bunda, Lydia Bupilipili amesema mafunzo hayo yanatarajiwa kuanza mapema mwezi wa tano hivyo waombaji watekeleze masharti hayo.
Amesema ni agizo la serikali kwamba hakuna atakayejiunga na jeshi la kujenga taifa(JKT) bila kupitia mafunzo ya mgambo na kwamba vijana waanze mchakato huo kutoka ngazi za vijiji.

“ Serikali imeamua kufanya hivi kwa sababu nafasi ya kujiunga na JKT inapotangazwa vijana wengi wanakosa sifa za kujiunga kutokana na sababu mbalimbali ambazo zinaweza kuondolewa mapema wanapopata mafunzo ya mgambo na sisi hatutaki vijana kukosa nafasi hizi za ajira” alisema Bupilipili.

Aidha ameeleza kuwa vijana wanaopitia mafunzo ya mgambo hupata nafasi ya ajira mbalimbali ikiwa ni pamoja na JKT, JWTZ, ulinzi katika makampuni na taasisi mbalimbali, ulinzi wa mitihani ya taifa na wakati wa uchaguzi na kwamba hakuna atakayepata nafasi hizo kama atakuwa mgambo asiye na sare zilizoidhinishwa na jeshi la ulinzi wa wananchi(JWTZ).


No comments:

Post a Comment