Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameiagiza
Takukuru imkamate na kumhoji meneja wa mkoa wa Wakala wa Majengo
Tanzania (TBA), Peter Salim baada ya kushindwa kutekeleza ujenzi wa
mradi wa ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Butiama.
Taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya
Waziri Mkuu imesema mtendaji huyo mkuu wa Serikali alisema licha ya
Serikali kutoa Sh600 milioni Aprili mwaka jana kwa ajili ya kuanza
ujenzi wa ofisi hizo, hadi sasa hakuna kilichofanyika.
Hata hivyo, meneja huyo katika alisema
maelezo yake alieleza kuwa hadi kukamilika ujenzi wa ofisi hiyo
utagharimu Sh3 bilioni na kwamba kati ya fedha zilizotolewa na Serikali,
Sh400 milioni zimetumika kujengea msingi, kauli ambayo ilipingwa na
mkuu wa wilaya hiyo, Anna-Rose Nyamubi.
“Waziri Mkuu si kweli kwamba kuna kazi
inayoendelea, bali kilichopo pale ni mashimo ambayo hayajulikani ni ya
nini. Pia, kuna jengo moja lilijengwa kwa mabati kama stoo hakuna
mafundi wanaoendelea na kazi,” alisema Nyamubi.
Majaliwa alisema Serikali ipo katika
mchakato wa kuboresha mazingira ya wafanyakazi, ikiwamo ujenzi wa ofisi
za watumishi na kwamba haitamvumilia mtu yeyote atayekwamisha juhudi
hizo.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu
amemuagiza kaimu katibu tawala wa Mara, Raphael Nyanda kutuma timu ya
wakaguzi kufanya ukaguzi maalumu katika ofisi ya mkurugenzi wa
Halmashauri ya Wilaya ya Butiama.
Alisema halmashauri hiyo imekuwa na tabia ya kutumia fedha za miradi ya maendeleo kwa shughuli nyingine.
Alikuwa akizungumza na watumishi na madiwani wa Butiama katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Mwalimu Nyerere.
Pia, Waziri Mkuu aliagiza kuchunguzwa
kwa Solomon Ngiliule, ambaye ni mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Masanja
Sabuni (mweka hazina) na Robert Makendo (ofisa ununuzi).
No comments:
Post a Comment