Matumaini bei ya pamba kupanda yazidi kufifia kwa wakulima mkoa wa Simiyu - Mazingira FM

Mazingira Fm Live

Breaking News

Monday 10 July 2023

Matumaini bei ya pamba kupanda yazidi kufifia kwa wakulima mkoa wa Simiyu

 

Wakulima wa pamba kijiji cha Sapiwi mkoani Simiyu wakiwa katika kituo cha ununuzi wa pamba kwa ajili ya kuuza. Picha na Edward Lucas

Ikiwa ni takribani miezi miwili tangu kuzinduliwa msimu wa pamba 2023 hakuna hata senti moja iliyoongezeka kutoka katika bei elekezi iliyotangazwa na serikali ya shilingi 1,060 kwa kilo.

Wakizungumzia hali hiyo wakati wa mahojiano na Mazingira Fm iliyotembelea vituo hivyo hapo jana tarehe 9 July 2023 baadhi ya wakulima na viongozi wa vituo vya ununuzi wa pamba katika kijiji cha Lutubiga, Mkula na Sapiwi mkoani Simiyu wamesema hali hiyo imefanya baadhi ya wakulima wauze pamba yao kwa shingo upande baada ya kusubiri pasipo mafanikio wala dalili yoyote ya bei kuongezeka.

Elias Joseph ambaye ni Mwenyekiti wa AMCOS kijiji cha Sapiwi amesema  Mkoa wa Simiyu wanatumia mfumo wa makampuni na Vyama vya Ushirika AMCOS katika ununuzi wa pamba ujulikanao kama 'Simiyu Model' lakini tangu uanze msimu wa pamba hakuna dhana ya ushindani wa makampuni katika kuongeza bei isipokuwa ushindani umebaki ni kwa wakulima kuangalia ni kituo gani kina mzani wa kuaminika na iwapo kina fedha za kumlipa kwa wakati.

"Wakulima walianza kwa kusuasua wakiamini huenda bei inaweza kuongezeka kama ilivyokuwa mwaka jana ambapo wakulima walianza na bei ya shilingi 1,560 kwa kilo na baadaye ilipanda hadi kufikia 2,200 lakini kwa mwaka huu hadi sasa bei imebaki ile ile iliyotangazwa ya 1060 na wakulima wameona hakuna namna bora wauze ili waendelee na mambo mengine" alisema Mashaka Kwisotela ambaye ni Katibu wa AMCOS kijiji cha Mkula.

Mashaka Kwisotela, Katibu AMCOS ya Mkula akiwa kwenye kituo cha ununuzi wa Pamba akiendelea na zoezi


Wakulima kijiji cha Sapiwi wakiendelea na zoezi la uuzaji wa pamba. Picha na Edward Lucas


No comments:

Post a Comment