Friday, 25 May 2018

WAKULIMA wa zao la pamba wilayani Bunda mkoani Mara hadi sasa wamegoma kuuza pamba zao kwa vyama vya msingi




WAKULIMA wa zao la pamba wilayani Bunda mkoani Mara hadi sasa wamegoma kuuza pamba zao kwa vyama vya msingi kwa kile wanachodai kuwa hawana imani na vyama hivyo ambavyo viliwadhuluma hapo awali.

Kitendo hicho kimewafanya baadhi ya mawakala wa makampuni waliojitayarisha katika vituo mbalimbali kushirikiana na vyama vya msingi kufunga virago vyao baada ya kukaa vituoni bila kuwaona wauzaji.

Hali hii imetokea katika vijiji vya Kunzugu, Bukole, Miale,Nyamatoke na baadhi ya maeneo huku wakiishutumu vikali serikali kuwa imechukua hatua za haraka kukabidhi majukumu hayo kwa vyama vya msingi kabla ya kufanya utafiti wa kina.

Aidha wakulima hao wamedai hawatauza pamba zao huku baadhi yao wakisema kuwa hali hiyo ikiendelea watahaahirisha kulima zao hilo katika msimu ujao na kwamba serikali inachangia kuandaa kifo cha zao hilo maarufu ya biashara.

Shija Maduhu(48) mkazi wa Kijiji cha Bukole akizungumza na mwandishi wa habari hizi alidai wakulima hawako tayari kuuza zao hilo kwa mfumo wa sasa hadi serikali ione umuhimu wa kufanya marekebisho.

“Tumetishwa na hali hii, kwanza vyama hivi vya msingi vya wakulima vilitunyanyasa sana katika kipindi kilichopita, fedha zetu zililiwa kwa mfumo huu………” alisema Maduhu.

“ we ni mwandishi wa habari, unajua wazi kwamba kutokana na mfumo huu wa kuuza zao lako na fedha kuchukuliwa baadaye wakulima walidhulumiwa mpaka mali ya vyama hivi vilitaifishwa kutokana na madeni, leo bila kupitia mchakato imara mfumo ule unarudishwa, kwa kweli serikali itusamehe katika hili.

“Mara Co-operative Union (MCU) kiko wapi, nani alikiua, tuna jineri hapa ya Ushashi bado iko chini ya mfilisi vyote vilivyouawa na mfumo huu wa vyama vya msingi…. Ni vyema serikali ingekaa nasi tujadiliane tufanye nini” alisisitiza.

Aidha alidai kitendo cha agizo la serikali la kutaka kila mkulima wa pamba afungue akaunti ili fedha za mauzo yake yatumwe kwenye akaunti yake inalenga fedha hizo kukatwa bila ridhaa za wakulima.
Wamedai walilima kwa furaha wakitegemea kupata fedha lakini matumaini yao yanaendelea kufifia huku wakikabiliwa na hali ngumu ya uchumi wakati ambapo wanafanya matayarisha ya kuwapeleka shule watoto katika muhula wa pili unaoanza mwezi Julai.

Hivi karibuni akifungua msimu wa mauzo ya pamba mkoani Mara katika Kijiji cha Bukole wilayani Bunda , mkuu wa mkoa wa Mara aliagiza kila mkulima wa pamba kuhakikisha anafungua akaunti benki ili atakapouza pamba yake fedha zake ziwekwe kwenye akaunti yake na si vinginevyo.

Pia Malima alitoa tahadhari kuwa mkulima yeyote ambaye atauza pamba zake holela au kwa kampuni yoyote bila kupitia vyama vya msingi atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Mkuu wa wilaya ya Bunda, Lydia Bupilipili na watendaji wake wilayani Bunda inawasisitizia wakulima wa Bunda kuuza pamba zao katika vyama vya ushirika ingawa toka msimu wa manunuzi ufunguliwe Mei Mosi mwaka huu bado wakulima wengi hawajauza pamba zao.

“Wazee wa Mila Tarime sasa tunaona Ukeketaji ni Kero”

                         

Mwenyekiti CCM Mara Kiboye atembelea Kijana aliyejenga Hoteli juu ya Mti...

                      

Pitia Habari Zilizopo Katika Magazeti ya Leo Ijumaa ya May 25




Thursday, 24 May 2018

Zahanati ya kijiji cha kurusanga iliyopo kata ya Salama wilaya ya Bunda Mkoani Mara kimepokea msaada wa Darubini kutoka kwa Diwani wa Kata ya Ketare


Zahanati  ya  kijiji cha kurusanga  iliyopo kata ya Salama wilaya ya Bunda  Mkoani  Mara  imepokea  msaada  wa Darubini kutoka kwa Diwani wa Kata ya Ketare mh.Mramba  Simba  Nyamkinda  itakayotumika kupima  magonjwa mbalimbali na kuboresha huduma katika  zahanati  hiyo.

Darubini hiyo  yenye thamani ya shiliingi milioni moja inayotumia nishati ya umeme na jua imetolewa  jana jumamosi na mh.Mramba  Simba  Nyamkinda  ambae ni diwani wa kata ya Ketare baada ya kuona ukosefu wa kifaa hicho katika zahanati hiyo. 

Akizungumza  wakati  wa kupokea kifaa hicho Daktari msimamizi wa Zahanati  hiyo  Sajadi Hassani  amemshukuru mheshimiwa Mramba ambapo amesema awali walikuwa wakitoa huduma kwa kukisia ugonjwa  lakini sasa darubini hiyo itawasaidia kubaini magojwa na kutoa huduma kwa uhakika.

Pia Mramba amemtaka daktari wa kituo hicho kutunza vizuri kifaa hicho  ili kiwasaidie  wananchi kupata huduma za vipimo  ambapo amewaomba  wasikipoteze kama walivyo poteza Darubini aliyoitoa hapo awali.

Wakati huo huo mh.Mramba ametoa pawa miksa katika kanisa la EAGT  la kurusanga na kuahidi kutoa mifuko kumi ya sementi ili kuendeleza ujenzi wa kanisa hilo.

Bulaya Aitupia Lawama Serikali....Adai Imesababisha TANESCO Ifiilisike

Mbunge Bunda Mjini (Chadema), Ester Bulaya amesema Serikali ya Awamu ya Tano tangu ilipoingia madarakani Novemba 5, 2015 imelifanya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kushindwa kujiendesha kwa faida, kutaka ligawanywe.

Bulaya ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Mei 24, 2018 bungeni mjini Dodoma katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Nishati mwaka 2018/19.

Amesema kwa muda mrefu ripoti mbalimbali za kamati za Bunge, ikiwamo ya mashirika ya umma, zinaeleza namna Tanesco inavyojiendesha kwa hasara.

Amesema kabla ya Serikali hiyo haijaingia madarakani, Tanesco ilikuwa ikipata hasara ya Sh124 bilioni lakini baada ya kuingia madarakani Tanesco inapata hasara ya Sh346 bilioni inayotokana na upugufu wa maji na gharama za uendeshaji.

“Tanesco ina madeni ambayo yamepanda kwa asilimia 23. Kabla Serikali hii haijaingia madarakani, Tanesco walikuwa na madeni ya Sh738 bilioni lakini baada ya kuingia yamefikia Sh958 bilioni na haya si maneno ya Bulaya. Ukiangalia ripoti ya CAG, inasema madeni hayana uhusiano kati ya Tanesco na mali, kwa maana nyingine Tanesco imefirisika,” amesema Bulaya.

Amesema wakati madeni haya yanatokea, kulikuwa na ushauri na mikakati mbalimbali ya kuligawanya shirika hilo ili kutenganisha usambazaji na uzalishaji.

“Leo hii tusingekuwa tunazungumza umeme wa vibaba wakati tunataka Tanzania ya viwanda. Wakati haya yanafanyika, Tanesco inashindwa kukusanya madeni makubwa, Tanesco inaidai Hospitali ya Tumaini Dola milioni 9.4 za marekani sawa na Sh18 bilioni na ni kodi ya pango,” amesema.

“Kodi hii ni tangu mwaka 1998 haijawahi kulipwa, kulikuwa na kesi mahakamani na Tanesco ikashinda na mahakama imeitaka kuondoka lakini mpaka sasa haijachukua hatua zozote.”

Mbunge huyo pia alihoji kitengo cha wizara hiyo kutenga Sh700 bilioni kwa ajili ya mradi wa umeme wa Stiegler’s Gorge badala ya fedha hizo kuzipeleka Rea (Wakala wa Umeme Vijijini) na Tanesco.

Monday, 21 May 2018

Serikali nchini Tanzania imeshauriwa kuchukua hatua za kisheria kwa wafugaji wanaobainika kuingiza mifugo yao katika hifadhi ya wanyama -Bunda


Serikali nchini Tanzania imeshauriwa kuchukua hatua za kisheria kwa wafugaji wanaobainika kuingiza mifugo yao katika hifadhi ya wanyama na mapori ya akiba badala ya kukamata na  kupiga mnada pasipo kufuata utaratibu stahiki.

Ushauri huo umetolewa hii leo na Musa Gedi Musa Wakili wa kujitegemea ambae pia ni mwalimu kitaaluma,ambapo amedai hakuna sheria ya nchi  inayoruhusu wafugaji kuuziwa mifugo yao kiholele isipokuwa ni kuchukuliwa hatua kwa kufikishwa mahakamani .

Amesema ni fedheha kuuzwa kwa shilingi elfu sabini ng’ombe mwenye thamani ya shilingi laki sita.

Akizungumzia changamoto zinazowakabili wafugaji kanda ya ziwa na hasa mkoani mara mwenyekiti wa chama cha wafugaji kanda ya ziwa Mrida mshota amesema kuwa wafugaji wamekuwa kama wahalifu .
 
Akitolea mfano wa athari ambazo wafugaji wamepata na  takwimu mbalimbali za wafugaji waliokamatiwa mifugo yao na kuuzwa kwa bei ya chini ikiwemo wilayani Serengeti amedai zaidi ya ng’ombe 200 walikamatwa wilayani Serengeti na kuuzwa kwa bei ya chini na kuongeza kuwa mfumo mzima wa mnada uligubikwa na rushwa.



Akatwa Koromeo Na Mumewe Kwa Wivu Wa Mapenzi

Mwanamke mmoja aliyefahamika kwa jina la Mary Miyombo (32), mkazi wa Kata ya Hombolo, Bwawani mkoani Dodoma   amenusurika kufa baada ya kukatwa koromeo na mumewe wake akiyejulikana kwa jina la Mgowela Anderson.

Chanzo cha kisa hicho kilichotokea Mei 16, mwaka huu kinaelezwa ni wivu wa kimapenzi ambapo inadaiwa mwanamke huyo alikutwa na mwanamume mwingine ndipo mumewe akamjeruhi kwa kumkata na panga kwenye koromeo na kukimbia.

Akizungumza kwa tabu huku akilia, Mary ambaye kwa sasa amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma   amesema siku ya tukio akiwa ametoka kuuza pombe kilabuni kijijini hapo alifika nyumbani kwake na kwenda anapoweka fedha zake ambapo aligundua 1,000 haipo jambo lililosababisha kumuuliza mume wake huyo.

“Nilipomuuliza tu kama amechukua hiyo hela ndipo kipigo kilipoanza hadi kufikia hatua ya kunikata na panga shingoni, yaani simtaki tena yule mwanamume kwani hii ni mara ya tatu ananipiga na kunijeruhi na nimekuwa nikimsamehe lakini kwa hili simtaki tena,” amesema Mary.

Mganga Mfawidhi wa hiyo, Caroline Damian amethibitisha kumpokea mgonjwa huyo hospitalini ambaye alilazwa wodi namba 10 na tayari amesharuhusiwa.

Hata hivyo, Kamanda wa polisi Mkoani Dodoma Gilles Muroto alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo hakupatikana.

Askofu wa kkkt aliyepigwa mawe aibiwa kiti.


Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Njombe, Isaya Mengele, amesema kuwa kitendo kilichofanywa na baadhi ya waumini wa kanisa hilo Dayosisi ya Ziwa Tanganyika kumjeruhi kwa kumpiga mawe Askofu wa KKKT Dayosisi ya Tanganyika, Ambele Mwaipopo,limelitia doa kanisa hilo na kinapaswa kulaaniwa.


Akizungumza jana katika ibada maalum iliyofanyika katika Kanisa la Kiaskofu la KKKT Usharika wa Sumbawanga Mjini, Askofu Mengele ambaye ni Mwenyekiti wa maaskofu wa KKKT Kanda ya Kusini, alisema ni aibu kubwa na fedheha kwa dayosisi hiyo yenye miaka minne tangu kuanzishwa kwake na waumini hao wanapaswa kutubu na kuomba radhi.


Alisema kuwa pia yeye ataongoza ujumbe wa maaskofu wa kanda hiyo kwenda kwa Rais John Magufuli kumuomba radhi kwa kitendo cha baadhi ya waumini hao kuvuruga amani ambayo serikali yake imekuwa ikiihimiza kwa kitendo cha kumjeruhi kwa kumpiga mawe Askofu Mwaipopo.


Pia Askofu alimshauri Askofu Mwaipopo kuvunja Baraza la Dayosisi hiyo kwa kuwa baadhi ya wajumbe wake wamekuwa ni chanzo cha mgogoro uliopo katika kanisa hilo na wamekosa utii kwake.


Muda mfupi kabla maaskofu sita wanaounda Kanda ya Kusini ya KKKT hawajafika kuongoza ibada ya jana na kumpa pole Askofu Mwaipopo kwa kujeruhiwa, baadhi ya waumini waliingia katika kanisa hilo na kuondoa kiti maalum cha kukalia askofu huyo wakati wa kuongoza ibada.


Maaskofu hao ni Renald Mtenji wa Ulanga Kilombero, Askofu Blastone Gaville (Dayosisi ya Dira-Iringa), Askofu Job Mbwilo (Dayosisi ya Kusini Magharibi- Matamba), Askofu Amon Mwenda (Dayosisi ya Ruvuma), Askofu Edward Mwaikali (Dayosisi ya Konde Mbeya) na Askofu Isaya Mengele (Dayosisi ya Kusini Njombe).


Lengo la jopo hilo la maaskofu hao limefika kumpa pole Askofu Mwaipopo na kuwasihi waumini waache mara moja vitendo vya uvunjifu wa amani kwa kuwa vinaliumiza na kulichafua kanisa hilo ambalo lina zaidi ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake nchini.


Katika ibada hiyo Katibu wa Dayosisi ya Ziwa Tanganyika, Fredrick Lazaro, alisoma tamko maalum la Halmashauri Kuu kwa wakristo wa Usharika wa Kathedral Sumbawanga Mjini kuekeleza waumini 21 na watumishi wa kanisa hilo kuwa wamejitenga na kanisa hilo kwa muda usiojulikana.


Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Dk. Alfan Haule, alisema vitendo vya uvunjifu wa amani havitafumbiwa macho na serikali na kama vitaendelea, itatumia vyombo vyake vya ulinzi na usalama kuvidhibiti.


Dk. Khaule aliagiza kuwa wote walioiba kiti cha Askofu Mwaipopo wasakwe na wakamatwe, ili wafikishwe mbele ya sheria wachukuliwe hatua kwani kitendo cha kuiba kiti hicho ni wizi kama wizi mwingine wowote.


Mei 7, mwaka huu, Askofu Mwaipopo alifukuzwa kwa mawe baada ya baadhi ya waumini kumzuia kuingia usharikani wakidai hawataki kumuona akiwepo eneo la kanisa la Usharika wa Simbawanga Mjini.