Lusato Masinde Afisa wanyamapori kutoka TAWA kanda ya ziwa ,picha na Catherine Msafiri
Kobe ni wanyama kama walivyo wanyamapori wengine na wanalindwa kisheria tuwatunze.
Na Catherine Msafiri,
Jamii imetakiwa kuendelea kuwatunza na kuwalinda kobe kwaajiri ya manufaa ya vizazi vijavyo kwani ujangili dhidi yao unahatarisha uwepo wa mnyama kobe kwa miaka ijayo.
Hayo yameelezwa na afisa wanyamapori kutoka TAWA kanda ya ziwa ndugu,Lusato Masinde alipofanya mahojiano na radio Mazingira fm kwenye kipindi cha uhifadhi na utalii.
Afisa wanyamapori TAWA kanda ya ziwa Lusato Masinde
Aidha Masinde ameeleza kuwa binadamu ndie kiumbe hatari zaidi kwa mnyama kobe kutokana na shughuli zao hasa pindi wanapochoma misitu Pia amebainisha kuwa mnyama kobe anafaida mbalimbali kiuchumi, kiikolojia na kijamii
Sauti ya Afisa wanyamapori kutoka TAWA kanda ziwa Lusato Masinde
Hata hivyo ameeleza sifa za mnyama kobe huku akibainisha kuwa kisheria watu wanaweza kuanzisha mashamba ya kufuga kobe isipokuwa tu kwa kuzingatia sheria na taratibu.
Sauti ya Afisa wanyamapori kutoka TAWA kanda ziwa Lusato Masinde
Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne kutoka Shule ya Sekondari Migungani wakiwa kwenye chumba cha kurushia matangazo radio Mazingira Fm
Wamesema kuwa ziara hiyo imewapanua uelewa wao kuhusu namna vyombo vya habari vinavyofanya kazi.
Na Taro Michael
Wanafunzi wa kidato cha nne kutoka Shule ya Sekondari Migungani, iliyopo wilayani Bunda, mkoani Mara, wamefanya ziara ya kielimu katika Redio Mazingira FM kwa lengo la kujifunza kwa vitendo kuhusu mawasiliano na utangazaji wa redio.
Ziara hiyo ni sehemu ya mtaala wa elimu unaolenga kuwajengea wanafunzi uelewa wa kina kupitia mafunzo ya vitendo, hasa katika masomo ya lugha, uraia, na teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA).
Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne kutoka Shule ya Sekondari Migungani wakiwa nje ya ofiza za radio Mazingira Fm
Wanafunzi hao takribani 20 walipata fursa ya kutembelea vitengo mbalimbali vya utangazaji, kujionea kwa macho namna vipindi vinavyoandaliwa, kurekodiwa na hatimaye kurushwa hewani. Pia walijifunza mbinu za ukusanyaji wa habari, uandishi wa taarifa na uhariri wa vipindi vya redio.
Aidha baadhi ya wanafunzi walieleza kufurahishwa na kile walichojifunza. Wamesema kuwa ziara hiyo imewapanua uelewa wao kuhusu namna vyombo vya habari vinavyofanya kazi na kuwaongezea ari ya kuchangia maendeleo kupitia fani ya mawasiliano.
Mkuu wa wilaya ya Bunda Mhe Aswege Enock Kaminyoge
Tangu kuanzishwa kwa jukwaa hili mwaka 2005 limesaidia wanawake wengi katika kuhakikisha wanazifikia ndoto zao
Na Adelinus Banenwa
Mkuu wa wilaya ya Bunda Mhe Aswege Enock Kaminyoge amezielekeza halmashauri za wilaya ya Bunda kuandaa program maalumu kwa ajili ya kutoa elimu ya mikopo kwa akina mama wajasiriamali ambao wanajiunga katika vikundi ili kupunguza changamoto za mikopo kwa akina mama hao
Dc kaminyoke ametoa maelekezo hay oleo may 8 2025 katika uzinduzi wa chemba ya wanawake wajasiriamali wilaya ya Bunda chini ya TANZANIA WOMEN CHEMBER OF COMARCE.
Sauti ya Mhe Aswege Enock KaminyogeBaadhi ya wanachama na wanufaika wa chemba TWCC
Baadhi ya wanachama na wanufaika wa chemba hiyo wamesema kuna fursa mbalimbali kwa wanawake kujiunga na umoja huo kutokana na kukutanishwa na wataalamu mbalimbali pamoja na taasisi za serikali zinazowapatia elimu ili kukabiliana na changamoto za kibiashara katika ujasiriamali wao
Aidha wametoa wito kwa wanawake wengine kutoogopa kujiunga na jukwaa hili kwa kuwa wapo walioanza pasipo kuwa na uelewa lakini hadi hivi sasa wametengeneza mtandao mkubwa wa biashara.
sauti ya wanufaika wa jukwaa la TWCCBaadhi ya wajasiriamali waliojiungq na jukwaa la TWCC wakionesha walivyoongeza thamani Bidhaa zao
Kwa upande wake mkurugenzi wa jukwaa hili la TWCC Maria Isidory amesema tangu kuanzishwa kwa jukwaa hili mwaka 2005 limesaidia wanawake wengi katika kuhakikisha wanazifikia ndoto zao katika kuwasaidia elimu ya biashara, mitaji na kuwakutanisha na wataalamu pamoja na taasisi za serikali kama vile TRA, SIDO miongoni mwa taasisi zingine
Sauti ya mkurugenzi wa jukwaa hili la TWCC Maria Isidory
Wateja wamepungua kwa kasi katika siku za hivi karibuni kutokana na watu wengi kuelekeza nguvu zao katika kununua samaki
Na Thomas Masalu
Imeelezwa kuwa katika mji wa Bunda, upatikanaji mkubwa wa samaki kwa sasa umeanza kuathiri kwa kiasi kikubwa biashara ya nyama ya ng’ombe, hali inayowatia hofu baadhi ya wafanyabiashara wa nyama hiyo.
Wafanyabiashara hao wamesema kuwa wateja wamepungua kwa kasi katika siku za hivi karibuni kutokana na watu wengi kuelekeza nguvu zao katika kununua samaki ambao wanapatikana kwa wingi sokoni.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti leo Mei 7, 2025, na redio Mazingira FM katika eneo la genge la jioni, wafanyabiashara hao wameeleza kuwa tofauti ya bei kati ya samaki na nyama ya ng’ombe imechangia kushuka kwa mzunguko wa biashara yao.
Wafanyabiashara hao wamesema kuwa licha ya changamoto hiyo, bado wana matumaini kuwa hali itabadilika pindi upatikanaji wa samaki utakapopungua.
Serikali tayari imetoa bilioni 53 kwa ajili ya ulipaji wa fidia kwa wakazi hao ili kuachia maeneo hayo yawe sehemu ya hifadhi ya taifa ya Serengeti.
Na Adelinus Banenwa
Wananchi wa Nyatwali ambao tayari wamelipwa stahiki zao kwa utaratibu wa kisheria watakiwa kuondoka.
Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa mkoa wa Mara Kanal Evance Mtambi katika kilele cha maadhimisho ya siku ya urithi wa dunia na afrika yaliyofanyika wilayani Serengeti mkoani Mara leo tarehe 5 May 2025.
Kanal Mtambi amesema serikali tayari imetoa bilioni 53 kwa ajili ya ulipaji wa fidia kwa wakazi hao ili kuachia maeneo hayo yawe sehemu ya hifadhi ya taifa ya Serengeti.
Baadhi ya wananchi waliohudhuria maadhimisho ya siku ya urithi duniani
Kanal Mtambi amesema eneo la Nyatwali tangu enzi za ukoloni lilionekana si sehemu salama kwa makazi ya binadamu na wakati huo lilitambulika kama guba ya speek na utaratibu wa wananchi waliokuwa eneo hilo kuhamishwa ulianza muda mrefu lakini serikali ya awamu ya sita imefanikisha jambo hilo.
Aidha mkuu wa mkoa wa Mara amesema kiasi cha malipo kilichosalia kinaendelea kulipwa kwa utaratibu uliowekwa
Ndege Makebe Karando (31) amuua kwa kumchoma visu aliyekuwa mpenzi wake ambaye ni muhudumu wa afya katika zahanati ya marambeka Zawadi John Kazi (35) kisha na yeye kujinyonga.
Na Adelinu Banenwa
Vilio na sintofahamu vimeendelea kutawala kwa wakazi wa kijiji cha Marambeka kata ya Ketare halmashauri ya wilaya ya Bunda kufuatia tukio la Ndege Makebe Karando (31) kumuua kwa kumchoma visu aliyekuwa mpenzi wake ambaye ni muhudumu wa afya katika zahanati ya marambeka Zawadi John Kazi (35) kisha na yeye kujinyonga.
Makebe Karando baba mzazi wa ndege amesema tukio hilo la kijana wake kufanya mauaji kisha na yeye kujinyonga limewaachia majonzi makubwa kutokana na wote waliopoteza maisha alikuwa akiwachukulia kama watoto wake.
Mama mzazi wa Ndege Makebe
Makebe amesema karando alikuwa na wake wawili lakini pia alikuwa na mahusiano na muhudumu huyo wa afya na tayari walishajitambulisha kwake na mara ya mwisho ilipotokea sintofahamu baina yao walimfikia na akawashauli na walimuhakikishia kuwa mgogoro umeisha hadi pale alipopata taarifa za tukio la mtoto wake Ndege kumshambulia Zawadi
Makebe anaeleza kuwa majira ya usiku alipokea taarifa za Zawadi kushambuliwa na Ndege lakini alikuwa hajamuona ndege japo taarifa za ujio wake pale kijijini alikuwa nazo kwa kuwa mtoto wake huyo anaishi maeneo ya Mugumu Serengeti ambako ana mke mwingine
Familia ya Ndege Makebe wakiwa msibani
Ameongeza kuwa wakati asubuhi kesho yake wanajiandaa kama nzengo kujikusanya ili waanze kumtafuta ndege na kumtia nguvuni kutokana na tukio alilolifanya ndipo alipopata taarifa kuwa mtoto wake huyo amekutwa shambani akiwa amejinyonga kwenye mti aina ya mkwaju na alpokwenda alishuhudia kweli Ndege amejinyonga
Makebe Karando
Ngei Mashoka rafiki wa karibu wa ndege ameiambia Mazingira fm kuwa aligundua kuwa rafiki yake amejinyonga baada ya kupigiwa simu kutoka Musoma kutoka kwa rafiki yao mwingine akidai amepokea simu kutoka kwa Ndege akidai anaenda kujiua kwa kujinyonga katika moja ya miti iliyo shambani mwake
Ngei Mashoka rafiki yake Ndege na liyegundua kuwa Ndege amejinyonga
Huku rafiki huyo akieleza kuwa maelekezo ya ndege yalikuwa endapo watamkuta ameshakufa wamtumie nauli mke wake aliyeko Mugumu aje kwenye msiba
Ngei Mashoka
Hata hivyo baadhi ya viongozi katika kijiji hicho akiwemo diwani wa kata ya Ketare Mramba Simba Nyamkinda na mwenyekiti wa kijiji Ramadhani Lukiko wamekemea tabia za vijana kujichukulia sheria mkononi huku wakitoa wito kuwa endapo kuna sintofahamu kwa watu wenye mahusiano ni vema wakapata suluhu kutoka kwa viongozi
viongozi diwani na mwenyekiti
Jeshi la polisi kupitia kwa kamanda wa polisi mkoa wa Para Pius Lutumo limethibitisha kutokea kwa matukio hayo mawili yaani kuuawa kwa Zawadi John na Ndege Makebe kujinyonga kwenye mti kwa kutumia shuka huku chanzo cha tukio hilo kikitajwa kuwa ni wivu wa kimapenzi baada ya marehemu Zawadi kukataa kuendelea kuwa na mahusiano na Ndege.
Zawadi John Kazi aliyekuwa muhudumu wa afya katika zahanati ya Marambeka inatajwa ameacha watoto wawili huku Ndege Makebe akitajwa kuacha wajane wawili na watoto watano
Katika utetezi wake mshitakiwa aliiomba mahakama imuachie huru kutokana na yeye kuwa ni mjane na ana watoto watano wanamtegemea.
Na Adelinus Banenwa
Mahakama ya wilaya ya Bunda imemuhukumu kifungo cha masharti (condition discharge) cha kutokutenda kosa lolote ndani ya miezi sita Neema Msimu John(28), Mkazi wa mtaa wa Mapinduzi kwa kosa la ukatali dhidi ya mtoto wake mwenye umri wa miaka minne kwa kumchoma moto kwenye mkono wake wa kushoto kwa kosa la kujisaidia hovyo.
Hukumu hiyoimetolewa na Hakimu mkazi Mwandamizi wa mahakama ya wilaya ya Bunda, Betron Sokanya, baada ya mshitakiwa kukiri kutenda kosa hilo ambalo ni kinyume na kifungu Cha 169A(1) na (2) cha kanuni ya adhabu sura ya 16 marejeo ya mwaka 2022.
Katika utetezi wake mshitakiwa aliiomba mahakama imuachie huru kutokana na yeye kuwa ni mjane na ana watoto watano wanamtegemea huku mmoja wapo akiwa ananyonya.
Neema Msimu John
Awali kabla ya hukumu kutolewa, mwendesha Mashtaka wa Jamuhuri Aristariko Msongelo ameiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa ili iwefundisho kwa jamii kuacha tabia ya ukatili dhidi ya watoto.
‘‘Naomba mahakama itoe adhabu kali kwa mshitakiwa ili iwe fundisho kwa jamii kuacha tabia ya ukatili dhidi ya watoto’’. Aristariko Msongelo mwendesha mashitaka wa Jamhuri Wilaya ya Bunda.
Aidha Afisa ustawi wa jamii Wilaya ya Bunda Florence Debogo awewaasa wazazi kutotumia adhabu kali kwa watoto na badala yake watumie adhabu mbadala kama kumnyima mtoto kuangalia television na kuto kwenda kucheza ili kupunguza wimbi la ukatili kwa watoto.