WAKAAZI WA TAMAU WAOMBA UONGOZI WA WILAYA YA BUNDA KUFIKA MARA KWA MARA ILI KUSIKILIZA KERO ZAO KATIKA MCHAKATO WA KUHAMISHWA - Mazingira FM

Mazingira Fm Live

Breaking News

Saturday 22 April 2023

WAKAAZI WA TAMAU WAOMBA UONGOZI WA WILAYA YA BUNDA KUFIKA MARA KWA MARA ILI KUSIKILIZA KERO ZAO KATIKA MCHAKATO WA KUHAMISHWA

 

Wananchi wa mtaa wa Tamau kata ya Nyatwali wakiwa katika mkutano kujadili hatima yao katika eneo hilo.


Wananchi wa Mtaa wa Tamau kata ya Nyatwali Halmashauri ya Mji wa Bunda Mkoani Mara wameuomba uongozi wa Wilaya hiyo kufanya mikutano ya mara kwa mara katika maeneo yao ili kuwawezesha kupata taarifa na ufafanuzi wa baadhi ya mambo yanayohusu mchakato wa kuhamishwa katika eneo hilo.


Wakizungumza katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na uongozi wa mtaa huo eneo la shule ya msingi Tamau jana tarehe 21 April 2023 wenye lengo la kuelimisha wananchi kufungua akaunti za benki na kuwapa taarifa juu ya utaratibu uliotolewa kwa wale wenye malalamiko mbalimbali, wananchi hao wamesema ni vema uongozi wa Wilaya ukawa na utaratibu wa kufika ili kuwasikiliza kama ilivyokuwa sehemu ya ahadi zao.




Mkaazi wa Tamau akichangia mawazo yake katika mkutano wa wananchi na viongozi wa mtaa huo.





Katika mkutano huo wananchi hao wamekuwa na hoja mbalimbali ikiwa ni pamoja na mchakato wa utathimini wa maeneo yao, kiwango cha fedha kinachopendekezwa, mchakato wa ufunguzi wa akaunti na mambo mengine ambayo bado wanaona licha ya majibu yanayotolewa kupitia uongozi wa mtaa huo bado wanaona kuna umuhimu kwa uongozi wa ngazi za juu kufika mara kwa mara ili kuwasikiliza.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa huo, Asafu Ernest Owiti amesema mtathimini mkuu wa taifa ameunda kamati inayoongozwa na Diwani wa kata hiyo huku katibu wake akiwa ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Bunda ili kufuatilia malalamiko mbalimbali ya wananchi kisha kutoa mapendekezo ambayo yatawasilishwa kwa mtathimini kwa hatua zaidi.


Mwenyekiti wa Mtaa wa Tamau, Asafu Ernest Owiti


Naye Afisa Mtendaji Mtaa wa Tamau, Dotto Mirumbe amesema katika mkutano walialika benki mbalimbali kufika ili kutoa elimu na maelekezo ya namna ya kufungua akaunti lakini wote wameshindwa kufika kutokana na sababu mbalimbali hivyo zoezi hilo litafanyika siku ya jumatatu tarehe 24 April 2023 hii ikiwa ni moja kati ya hatua ya kutoa ufumbuzi kwa baadhi ya maswali inayoibuka kwa wananchi hao.

Dotto Kihiri Mirumbe, Afisa Mtendaji Mtaa wa Tamau akitoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja kwa wananchi wa Tamau.


Baadhi ya wananchi wakiwa wanafuatilia mkutano wakiwa nje baada ya chumba cha darasa kukosa nafasi













No comments:

Post a Comment